Mwenge wa Uhuru Ulipokelewa Wilaya ya Gairo tarehe 22.07.2018,eneo la Kijiji cha Tabu-Hotel ukitokea Manispaa ya Morogoro na kukimbizwa kupitia barabara ya Morogoro-Dodoma,Ngiloli-Idibo na barabara za katikati ya Mji wa Gairo.
Mwenge ulitembelea jumla ya miradi sita (6) katika umbali wa km. 72.0. ukipita katika kata za Chigela, Kibedya, Chakwale, Madege, Idibo, Magoweko, Ukwamani na Gairo.
Miradi hiyo ni:
Ujenzi wa Shule ya Sekondari ya Chakwale “B” ulianza mwezi Mei, 2018 kwa lengo la kuanzisha Shule mpya ya Sekondari baada ya Kata ya Chakwale kugawanywa na Shule ya Sekondari ya Chakwale iliyokuwepo kubaki katika Kata ya Madege na kuiacha Kata ya Chakwale bila shule ya Sekondari.
Lengo la mradi ni kujenga madarasa manne (4) kwa awamu ya kwanza. Miundombinu mingine ihusuyo ukamilifu wa shule ya sekondari itaendelezwa baada ya awamu hii kukamilika.
Hadi sasa ujenzi upo katika hatua za awali za ujenzi wa msingi kwa madarasa manne (4) ya kidato cha kwanza hadi cha nne.
Mradi huu unatarajia kugharimu jumla ya Tshs. 83,740,500 kutoka Serikali Kuu, Halmashauri, Nguvu kazi na michango ya wananchi. Tayari wananchi wamechangia kiasi cha Tshs. 16,490,000.00 zimetumika. Na faida za Mradi ni:
i. Kufuatia mafanikio makubwa ya Mpango wa Elimu Bila Malipo na mwitikio mkubwa wa wanafunzi kujiunga na shule za msingi, Mradi huu utakuwa na manufaa makubwa katika kuongeza wigo wa kuwapokea wanafunzi wengi zaidi wanaomaliza shule za Msingi.
ii. Huduma ya elimu ya Sekondari itakuwa imesogezwa karibu zaidi na jamii na hivyo kupunguza changamoto mbalimbali wanazokumbana nazo wanafunzi pale wanapotembea umbali mrefu kufuata huduma hii Kata nyingine hasa kipindi cha mvua.
Mwenge wa Uhuru umepitia kwenye mradi huu kwa ajili ya kuuona
Mradi wa Shamba la Mbegu za Mihogo katika kijiji cha Sanganjeru uliopo katika Kata ya Madege.
Mradi ulianza mnamo mwaka 2018 baada ya kupokea mbegu za muhogo aina ya Kiroba kiasi cha vipande 28,000 kutoka Kituo cha Utafiti wa mazao ya Kilimo Kanda ya Mashariki Ilonga, Kilosa Morogoro. Ushirikiano na Halmashauri ya Wilaya ya Gairo. Mradi ulianza kwa kuwaelimisha wana kikundi juu ya umuhimu wa uzalishaji wa mbegu ambapo kitakuwa chanzo kikubwa cha kuwaongezea kipato kwa kuuza mbegu zitakazopatikana na wao kuzalisha mihogo ambayo inauhitaji mkubwa kwa walaji waliopo ndani na nje ya Wilaya.
Kikundi hiki cha JUHUDI kina wakulima 14 (wanaume 9 nawanawake 5) na nje vikundi 10 vya wakulima katika vijiji vitano ambavyo ni Meshugi, Malimbika, Nguyami, Madege na Ng’holongo.
Lengo kuu la mradi huu ni kueneza mbegu bora za muhogo ambazo zitasaidia sana kupambana na zao lenye uwezo mkubwa wakuhimili mabadiliko ya tabia nchi na kukinzana na magonjwa ya mimea na wadudu wa haribifu ili hatimaye kuwa na uhakika wa chakula, lishe na kuongeza kipato cha familia.
Mbegu za mihogo vipande 28,000 vimepandwa katika eneo la ekari 7 (hekta 2.8) ikiwa ekari 5 zimepandwa katika matuta na ekari 2 kilimo cha sesa ili kuona uwiano wa tija katika aina zote za kilimo.
Kila ekari imechukuwa vipande 4,000 katika nafasi ya mita 1 kwa mita 1 au (sentimita 100 x sentimita 100), Mbegu hizi zilipandwa tarehe 20 mpaka 25 Machi, 2018 ambapo inategemewa baada ya miezi nane mpaka kumi hukaa kwenye shamba la mbegu na kuanza kusambazwa kwa wakulima.
Ni mategemeo ya Mradi huu kuzalisha jumla ya mbegu 672,000 za mihogo ambazo zitatosha kuzalisha ekari 168 (Hekta 67.2) za mihogo.
Mbegu za mradi huu zimetolewa bure na Serikali kupitia Kituo cha Utafiti wa mazao ya Kilimo Kanda ya Mashariki Ilonga, Kilosa Morogoro kwa ajili ya kuwapatia wananchi ili waweze kukuza na kuzalisha zao la muhogo. Katika gharama za mbegu na kuhudumia shamba, mradi huu umegharimu jumla ya Tsh 2,500,000 kama ifuatavyo:
Uboreshaji wa miundombinu katika kituo cha Afya Gairo kwa ujenzi wa majengo matano (5) ambayo ni Jengo la maabara, Wodi ya wazazi, Jengo la Upasuaji, Nyumba ya Mtumishi wa Afya na jengo la kuhifadhia maiti. Mradi huu upo Kata ya Magoweko.
Ujenzi wa Mradi wa Majengo ya Kituo cha Afya cha Gairo ulianza mnamo mwezi Machi, 2018 kwa lengo la kuboresha huduma za afya katika Wilaya ya Gairo. Lengo kuu la mradi huu ni kuboresha huduma za Afya kwa wananchi na kupunguza msongamano wa wagonjwa kituo cha Afya Gairo. Ujenzi upo katika hatua za umaliziaji
Mradi huu umetengewa na Serikali jumla ya Tshs 400,000,000.00. Fedha zote zimetolewa na hadi kufikia hatua hii, jumla ya Tsh. 323,617,776.58 zimeshatumika.
Mradi huu utaboresha hali ya utoaji wa huduma za Afya kwa wananchi na hasa kupunguza vifo vya akina mama na watoto. Utaboresha na kuimarisha huduma za upasuaji na maabara ambazo kwa sasa zinafanyika kwa kiwango kidogo.
Mradi huu utapunguza msongamano wa wagonjwa uliopo kwa sasa katika kituo cha Afya Gairo.
Mwenge wa Uhuru umepitia mradi huu wa uboreshaji wa miundombinu ya Afya kwenye Kituo cha Afya Gairo kwa ajili ya kuweka Jiwe la Msingi.
Ujenzi wa Hosteli ya Wasichana ya Triple G, Mradi huu upo kata ya Ukwamani.
Mradi wa Ujenzi wa Hosteli ya wanafunzi ijulikanayo kama Triple G yaani Gairo Girls Guide ni mtu binafsi aliyeamua kuwekeza katika elimu. Ujenzi wa Mradi huu ulianza mwezi Oktoba, 2017 kwa lengo la kutoa huduma kwa wanafunzi wa kike wanaotembea umbali mrefu kwa ajili ya kufuata elimu hasa katika shule ya Sekondari Sekwao.
Lengo kuu la mradi huu ni kuwapa wanafunzi wa kike elimu bora na kupunguza usumbufu wanaopata kwa kutembea umbali mrefu kwenda shuleni. Hadi sasa ujenzi upo katika hatua za ukamilishaji. Mradi huu mpaka utakapokamilika utagharimu kiasi cha Tshs 190,000,000.00 na tayari umeshagharimu kiasi cha Tshs. 90,000,000.00
Mradi utakapokamilika wanafunzi wa kike watapata huduma nzuri ya malazi ambayo itawawezesha kutulia na kufanya vizuri katika masomo yao. Mradi huu utasaidia katika kupambana na changamoto mbalimbali wanazokutana nazo wanafunzi wa kike hasa mimba za utotoni zinazotokana na mazingira wanayopita wakati wa kwenda na kutoka shuleni. Uwepo wa mazingira tulivu ya kujifunzia.
Mwenge wa uhuru utapitia kwenye mradi huu kwa ajili ya kuweka jiwe la Msingi
Ujenzi wa Ofisi ya TARURA na Mradi huu upo kata ya Ukwamani pia Ujenzi wa Ofisi ya Tarura katika Wilaya ya Gairo ulianza tarehe 20 Februari, 2018, kwa lengo la kupunguza gharama za upangishaji wa ofisi zinazotumika na TARURA.
Lengo kuu la mradi huu ni kuwahudumia wafanyakazi wa TARURA wapatao 19 na kupunguza usumbufu wanaopata kwa kukosa miundombinu ya ofisi. Aidha, uwepo wa Ofisi hii utasogeza huduma karibu zaidi kwa wananchi na hadi sasa ujenzi upo katika hatua za ukamilishaji na mpaka kufikia hatua hii umeshagharimu jumla ya Tshs 51,512,000.00.
Wafanyakazi wapatao 19 watatumia Ofisi hii na itawawezesha kutoa huduma iliyo bora na kupunguza usumbufu kwa wananchi wanaofika katika ofisi ya TARURA kupata huduma.
Mwenge wa uhuru utapitia kwenye mradi huu kwa ajili ya kuweka jiwe la msingi.
Aidha mkesha wa Mwenge ulikuwa katika Uwanja wa Soko la Mhindi Ukwamani .
Mwenge wa Uhuru ulitembea umbali wa Km. 81 kuelekea kijiji cha Dakawa Wilaya ya Mvomero kwa ajili ya makabidhiano tarehe 23/07/2018 ambapo Mkuu wa Wilaya ya Gairo Mh.Siriel S. Mchembe alimkabidhi Mkuu wa Wilaya ya Mvomero tarehe 23/07/2018.
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya Gairo-Mtaa wa Malimbika, Kata ya Gairo.
Sanduku la Posta: 40, GAIRO
Simu ya Mezani: +255 715240010
Simu ya Kiganjani: +255 715240010
Barua pepe: ded@gairodc.go.tz, info@gairodc.go.tz
Hakimiliki©2018 Halmashauri ya Wilaya ya Gairo. Haki Zote Zimehifadhiwa